Friday, May 29, 2015

UAINISHAJI WA NGELI ZA NOMINO KWA KUTUMIA KIGEZO CHA KIMOFOLOJIA



Swali. Kwa kutumi mifano ainisha ngeli za nomino za Kiswahili kwa kigezo cha kimofolojia kisha
           jadili upungufu wa uainishaji huo.

Istilahi Ngeli imechukuliwa kutoka ligha ya kihaya (Tanzania). Katika lugha ya kihaya neno ngeli lina maana ya aina ya kitu.
Tuki (1990), wanaeleza kuwa Ngeli za nomino ni kundi moja la majina yaliyo na upatanisho wa kisarufi unaofanana na viambishi vya umoja na wingi vinavyofanana. Kwa mujibu wa fasili hii ngeli za nomino ni kundi la nomino zilizo na:
·         Upanisho wa kisarufi unaofanana (kisintaksia), na
·         Viambishi vya umoja na wingi vinavyofanana (kimofolojia).
Kamusi ya Kiswahili sanifu (1981), inaeleza kuwa ngeli za nomino ni utaratibu wa taaluma ya sarufi ya lugha katika kupanga aina za majina. Fasili hii ina upungufu kwa sababu tunaamini kuwa ngeli ni kundi la nomino za aina moja na ndio ule utaratibu wa kupanga nomino katika makundi kama fasili ya hapo juu inavyodai.
Kwa ujumla ngeli za nomino ni utaratibu unaotumika kupanga nomino za lugha katika makundi mbalimbali kwa kufuata vigezo vya kisarufi katika lugha ya kiisimu.
Kigezo cha kimofolojia ni kigezo ambacho huzingatia zaidi viambishi awali vya umoja na wingi lakini mzizi na viambishi tamati havihusishwi. Nomino zilizo na viambishi vya mwanzo vilivyosawa huwekwa katika ngeli moja. Ngeli za nomino huwa na sehemu mbili kimuundo ambazo huwa ni mwanzo na shina. Mwanzo huwa ni kiambishi awali na shina hujumuisha mzizi wa neno na kiishio ambacho huwa ni mofimu inayotumiwa kuunda nomino. Kiambishi awali ambacho hutumika kuainishia ngeli huitwa kiambishi ngeli.
Kwa kutumia kigezo cha kimofolojia ngeli za nomino za Kiswahili zimeainishwa katika makundi mbalimbali kwa kurejelea hali ya umoja na wingi wa nomino husika. Katika kigezo hiki kila kiambishi ngeli hupewa namba ya kukitambulisha. Kigezo hiki kimejadiliwa na wataalamu mbalimbali na miongoni mwao ni Mgullu na Habwe na Karanja.
Kwa kuanza na Mgullu (2001), katika kuainisha ngeli za nomino anazingatia zaidi viambishi awali vya idadi ya umoja na wingi katika nomino hizo. Mzizi na viambishi tamati katika nomino hizo huwa havihusishwi hata kidogo. Aidha viambishi awali vinavyotumika ni vile vya umbo la kawaida la nomino siyo viambishi awali vya ukubwa au udogo wa nomino hizo. Ngeli tutakazopata hapa zitakuwa ngeli za nomino za kimofolojia tofauti na ngeli za nomino za kisintaksia. Kwake yeye kundi moja la nomino zilizo na viambishi awali vya umoja na/au wingi vinavyofanana au nomino zilizo na viambishi awali hata kimoja huwa na ngeli yao. Yeye aliainisha makundi makuu manne ya ngeli za nomino kimofolojia ambayo ni; ngeli sita za nomino zilizo na viambishi awali vyote viwili yaani umoja na wingi, ngeli moja ya nomino zilizo na kiambishi awali cha umoja tu pamoja na mofu kappa ya wingi, ngeli moja ya nomino zilizo na kiambishi awali cha wingi tu pamoja na mofu kapa ya umoja, na ngeli moja ya nomino zisizo na kiambishi chochote. Kwa ujumla anaainisha ngeli za nomino tisa ambazo ni kama ifuatavyo:
1)      Ngeli ya MU-WA
Katika ngeli hii zipo nomino zilizo na kiambishi awali {MU} katika umoja na kiambishi awali {WA} katika wingi. Kwa mfano
                                                Umoja                                                                         wingi
                         Mu + tu (mtu)                                                                        watu
                         Mutoto (mtoto)                                                          watoto
                        Muungwana                                                                waungwana
                        Muana (mwana)                                                         wana
Mofu (MU) ya umbo halisi la umoja katika ngeli huweza kudhihirishwa katika maumbo mbalimbali kama vile {M, MU na MW}.
2)      Ngeli ya M-MI
Ngeli hii ina nomino ambazo hutumia kiambishi awali {M} katika umoja na {MI} katika wingi.
Kwa mfano;     umoja                                                  wingi
                                    M + ti                                                  mi + ti
                                    M + tume                                            mi + tume
                                    M + chungwa                                      mi + chungwa
                                    M +chezo                                            mi + chezo
3)      Ngeli ya JI-MA
Katika ngeli hii zipo nomino zilizo na kiambishi awali cha umoja {JI} na kiambishi awali cha wingi {MA}. Kwa mfano:
                                    Umoja                                                             wingi
                                    Jicho                                                    macho
                                    Jiwe                                                     mawe
                                    Jino                                                      meno
                                    Jiko                                                      maiko (meko).
4)      Ngeli ya KI-VI
Katika ngeli hii zipo aina za nomino zilizo na kiambishi awali cha umoja {KI} na kiambishi awali cha wingi {VI}. Kwa mfano:
                                    Umoja                                                             wingi
                                    Kiti                                                       viti
                                    Kiatu                                                    viatu
                                    Kiumba (chumba)                               viumba (vyumba)
                                    Kiakila (chakula)                                 viakula (vyakula).
Hapa umbo {KI} kiambishi awali cha umoja, lina alomofu mbili yaani {Ki} na {Cha} na umbo {VI} la wingi lina alomofu {Vi} na {Vy}.
5)      Ngeli ya U-N
Katika ngeli hii kuna nomino zenye kiambishi awali {U} umoja na {N} wingi. Kwa mfano:
                                    Umoja                                                             wingi
                                    Udevu                                                  ndevu
                                    Udago                                                  ndago
                                    Udara                                                  ndara
                                    Ulimi                                                   ndimi
                                    Ubawa                                                 mbawa
Tunaona hapa kuwa {N} umbo la wingi lina alomofu mbili yaani {N} na {M} katika muktadha maalumu.
6)      Ngeli ya U-MA
Katika ngeli hii {U} ni kiambishi cha umoja na {MA} ni kiambishi cha wingi. Kwa mfano:
                                    Umoja                                                             wingi
                                    Ugonjwa                                              magonjwa
                                    Uasi                                                     maasi
                                    Upishi                                                  mapishi
                                    Uamuzi                                                maamuzi.
7)      Ngeli ya U- Ø 
Ngeli hii hujumuisha maneno ambayo kiambishi awali umoja huwa ni {U} na kiambishi awali wingi mofu kappa{ Ø}. Kwa mfano:
                                    Umoja                                                             wingi
                                    Ukuta                                                   Ø + kuta (kuta)
                                    Ukucha                                                Ø + kucha (kucha)
                                    Upande                                                Ø + pande (pande).
8)      Ngeli ya Ø-MA
Katika ngeli hii mofu kappa { Ø} huwakilisha umoja na mofu {ma} huwakilisha wingi. Kwa mfano:
                                    Umoja                                                             wingi
                                    Ø debe                                                            madebe
                                    Ø kasha                                               makasha
                                    Ø jembe                                              majembe
                                    Ø bepari                                              mabepari.
9)      Ngeli ya Ø-Ø
Nomino zilizo katika ngeli hii ni zile ambazo hazina kiambishi idadi hata kimoja. Maumbo ya nomino hizi hayaoneshi idadi (umoja na wingi) katika maumbo yake. Kwa mfano:
                                    Umoja                                                 wingi
                                    Taa                                                      taa
                                    Saa                                                      saa
                                    Kuku                                                    kuku
                                    Ng’ombe                                             ng’ombe
                                    Nyumba                                               nyumba
                                    Samaki                                                            samaki.
Baada ya kuona uainishaji wa ngeli za nomino kwa kutumia kigezo cha kimofolojia kwa mujibu wa Mgullu, tutazame uainishaji wa ngeli hizi kwa kutumi kigezo hikihiki cha kimofolojia kwa mujibu wa Habwe na Karanja (2012). Wao wanaainisha ngeli za nomino kwa kuzingatia kufanana kwa viambishi vya mianzo ya nomino. Nomino zenye viambishi awali vilivyosawa huwekwa katika ngeli moja. Wao wanaainisha ngeli zifuatazo:
1.      Ngeli ya {MU}
Ngeli hii huchukua nomino zenye kiambishi ngeli {mu} pamoja na alomofu zake.
Kwa mfano; {MU} m- motto, mtu,
                             mu- muungwana, muuaji na
                             mw- mwalimu.
2.      Ngeli ya {WA}
Hii ni ngeli yenye kundi la wingi wa ngeli ya kwanza. Kwa mfano:
                        {WA} - watoto, watu, waungwana, wauaji na waalimu.
3.      Ngeli ya {M}
Ngeli hii ni ya umoja ambayo pia ina alomofu zake tatu yaani m, mu na mw. Kwa mfano:
                        Mut i- mti
                        Muembe - mwembe
                        Mundi – mundi.
{mw} hutokea ikiwa shina la nomino linaanzia na vokali [u], huwa {m} ikiwa shina la nomino linaanza na konsonanti na huwa {mu} ikiwa shina la nomino linaanza na vokali [u].
4.      Ngeli ya {MI}
Ngeli hii huchukua wingi wa ngeli ya tatu. Kwa mfano:
                        Miti, migomba, miembe na miundi.
5.      Ngeli ya {JI/Ø}
Mofu ya ngeli hii huwa ni {ji}. Kwa mfano jitu, jicho, Øgoti, na Øtawi. Kuna nomino zingine huunganishwa katika kundi hili japo hazina umbo dhahiri lililotajwa kwa maana zina mofu kapa. Nomino hizi huunganishwa katika kundi hili kwa sababu zenyewe wingi wake unaingiliana na ule wa kundi hili unaodhihirishwa katika ngeli ya sita.
6.      Ngeli ya {MA}
Ngeli hii huwakilisha wingi wa ngeli ya tano. Kwa mfano: macho, magoti, matawi na majitu.
7.      Ngeli ya {KI}
Mofu ngeli {ki} huwa na alomofu {ch} kutokana na kanuni za kifonolojia (ukaakaishaji). Kwa mfano nomino katika kundi hili ni: kiatu, kitu, kisu na kiakula (chakula).
8.      Ngeli ya {VI}
Ngeli hii huonesha wingi wa ngeli ya saba kwa mfano viatu, vitu, visu na viakula (vyakula). Ngeli hii ina alomofu {vy}.
9.      Ngeli ya {N/Ø}
Ngeli hii huhusisha majina yanayoanza na N na kufuatiwa na konsonanti. Kwa mfano nyumba, nguzo na nguo.
10.  Ngeli ya {N/Ø}
Ngeli hii huwakilisha wingi wa ngeli ya tisa {n} japokuwa hakidhihiriki kaika maneno mengi ya ngeli hii. Ngeli ya tisa na kumi hudhihirika zaidi kisintaksia na siyo kimofolojia tu.
11.  Ngeli ya {U}
Nomino zenye kiambishi cha umoja {u} kwa mfano ulimi na ugonjwa huingia katika kundi hili. Pia ngeli hii ina alomofu {w} kwa mfano maneno kama: uembe (wembe) na uaraka (waraka).
12.  Ngeli ya {KA} kwa mfano katoto na kagari.
13.  Ngeli ya {TU}
Ngeli hii inawakilisha wingi wa ngeli ya 12. Kwa mfano: tu + toto na  tu + gari. Pia ngeli hii huwa na alomofu {tw}. Kwa mfano: twana na twalima (tuana na tualima).
14.  Ngeli ya {U} kwa mfano u + zuri na u + tukufu.
15.  Ngeli ya {KU}
Ngeli hii hurejelea vitenzi vinavzofanya kazi kama nomino. Kwa mfano: kuimba, kucheza na kuruka.
16.  Ngeli ya {PA}
Ngeli hii huonesha mahali kamili au mahususi kwa mfano: pale, ndani na hapa.
17.  Ngeli ya {KU}. Ngeli hii huonesha mahali kwa ujumla kwa mfano huku.
18.  Ngeli ya {MU}. Ngeli hii huonesha undani wa mahali kwa mfano humu, na mule.
Baada ya kuona uainishaji wa ngeli za nomino kwa kutumia kigezo cha kimofolojia kwa mujibu wa wataalamu mbalimbali, ufuatao ni upungufu wa kigezo hiki:

Muingiliano wa ngeli kwa mfano ngeli ya 1. Umoja na ya 2. Umoja ambapo kiambishi au mofu yake ni {m}. Kwa mfano katika maneno kama vile: mtu, mwana, mtoto na muungwana katika ngeli ya kwanza umoja na mti, mtume, mchungwa na mkono katika ngeli ya pili. Hali hii ya muingiliano inatokea pia katika ngeli ya 3 na 6 wingi, na ngeli ya 5, 6 na 7 umoja. Hii ni kwa mujibu wa mgullu (2001).
Kuna baadhi ya ngeli zinaonesha kiambishi kimoja tu aidha cha wingi au umoja. Kwa mfano kwa mujibu wa uainishaji wa Mgullu (2001) katika ngeli ya 7. {U- Ø} na ngeli ya 8. { Ø-MA}. Ngeli hizi hazina viambishi vya upande mmoja kwa mfano katika ngeli ya saba wingi na ngeli ya nane umoja.
Ngeli ya 9. (Ø - Ø) kwa mujibu wa mgullu (2001) haina kiambishi chochote aidha cha umoja au wingi. Huu ni udhaifu mwingine kwa kua msingi wa uainishaji huu (uainishaji wa kimofolojia) huzingatia viambishi awali vya umoja na wingi katika nomino ambavyo hufanana na kisha kuziweka  nomino hizo pamoja katika ngeli moja.
Uainishaji huu unachanganya nomino zisizo na uhai na zile zenye uhai. Kwa mfano kwa mujibu wa Mgullu (keshatajwa), katika ngeli ya nne kuna majina ya viumbe wenye uhai na vitu visivyo na uhai kwa mfano: kiti/viti, kiatu/viatu na kiumba (chumba)/viumba (vyumba) hizi ni nomino za vitu visivyo na uhai. Kwa upande mwingine nomino za vitu vyenye uhai ambazo huwekwa katika kundi hili ni kama vile: kiongozi/viongozi, kipofu/vipofu, kilema/vilema na kijana/vijana.
Kigezo hiki kinajihusisha na maumbo ya umoja na wingi tu na kutupilia mbali upatanisho wa kisarufi.
Pia udhaifu mwingine wa uainishaji wa ngeli za nomino kwa kutumia kigezo hiki cha kimofolojia, wataalamu wanatofautiana katika idadi ya ngeli. Kwa mfano Mgullu (keshatajwa) anaainisha ngeli tisa wakati Habwe na Karanja (wameshatajwa) wanaainisha ngeli kumi na nane.


MAREJELEO

Habwe, J. & Karanja, P. (2012). Misingi ya Sarufi ya Kiswahili. Nairobi: Phoenix Publishers.
Mgullu, R.S. (2001). Mtalaa wa isimu. Nairobi: Longhorn Publishers Ltd.

No comments:

Post a Comment